Serikali kutunga sheria kudhibiti uhalifu mtandaoni

Serikali inatarajia kuwasilisha bungeni,muswada wa sheria itakayodhibiti na kulinda taarifa za watu binafsi wanapowasiliana kwa simu za mkononi na kwenye intaneti.

Akifungua mkutano wa mwaka wa benki na wadau wa kupambana na uhalifu kwa kutumia mitandao, Mkurugenzi wa Teknolojia wa Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Dk Zaipuna Yonah, alisema kuwapo kwa sheria hiyo kutasaidia kuzuia watu kufuatilia mawasiliano binafsi katika mitandao ya simu na hata mawasiliano ya njia ya baruapepe.

Hivi karibuni kumekuwa na matukio kadhaa ya watu kuweka hadharani na hata kuchapisha mawasiliano ya watukatika magazeti na mitandao ya kijamii, kitendo ambacho kimelalamikiwa.

Miswada inayoandaliwa ni pamoja na sheria ya kulinda mawasiliano ya mtu binafsi, sheria ya kusimamia uhamishaji wa fedha kwa njia ya simu na sheria ya kushughulikia wale wanaofanya uhalifu kwa kutumia kompyuta.

Yonah alisema wanataka kuona sheria hizo zikipitishwa katika kipindi cha mwaka mmoja.
“Mapendekezo haya, hata hivyo, yana changamoto zake kwa kuwa sheria hizo zinaingiliana na utendaji wa vyombo vya habari.

“Kuna tatizo kwa kuwa unavyotaka kuzuia habari, vyombo vya habari navyo vinataka habari,” aliongeza.

Alisema mbali na kupendekeza kuwapo kwa sheria zitakazoratibu huduma ya mitandao nchini, Serikali pia inatarajia kuunda chombo kitakachokuwa kikisimamia watoa huduma wa mitandao kwa kuwapa vyeti vya utambuzi wa kazi zao.

“Tunatarajia kuwa na timu ya wataalamu wa kompyuta ambao watakuwa wanashughulikia iwapo kuna matatizo ya uhalifu wa kimtandao,” alisema.

Dk Yonah alisema Serikali imechukua hatua hizo kutokana na kupokea malalamiko mengi ya watu walioathirika na uhalifu wanaofanyiwa kupitia kwenye mitandao ya kompyuta.

Pia katika siku za karibuni kumejitokeza tatizo la wizi kwa njia ya ATM na hata kwenye uhamishaji fedha kwa njia ya simu za mikononi.

Akizungumzia mada juu ya mwelekeo wa malipo kwa njia ya teknolojia kwenye masoko yanayochipukia, Makamu wa Rais wa VeriFone kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati, Martin Holloway, alisema asilimia 10 ya watu wa eneo hili wanamiliki akaunti za benki wakati asilimia 60 wanamiliki simu za mkononi hivyo yanahitajika marekebisho ya haraka katika kudhibiti uhamishaji holela wa fedha kwa njia ya mtandao.

Alisema kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa na Taasisi ya Data Breach ya mwaka 2011, asilimia 78 ya uhalifu uliofanyika duniani kote ulihusu kuhamisha malipo kwa njia ya kompyuta au kwa njia ya simu za mikononi

Rais Kikwete awaongoza watanzania Katika Maadhimisho ya Miaka 49 ya Muungano