Afukuzwa kazi kwa kukutwa na shuhuda za BwanaYesu Asema yupo tayari hata kufa akimtetea Yesu

Mtaalamu mmoja wa utafiti katika Chuo Kikuu cha Ubelgiji amefukuzwa kazi kwa kosa la kukutwa na shuhuda za watu walioponywa na Bwana Yesu baada ya kuombewa katika makanisa ya kipentekoste.

Jambo la kustaajabisha zaidi ni kuwa mtaalamu huyo, Bw. Fernando Pauwels, alifukuzwa bila kupewa hata onyo, licha ya kufanya kazi kwa uaminifu kwa miaka 11, mfululizo.

Kwa mujibu wa taarifa za Shirika Habari la CBN (CBN News) Bw. Pauwels, alikuwa mtumishi mwandamizi katika Chuo Kikuu cha Katoliki kiitwacho  Leuven, ambacho ni miongoni mwa vyuo  vile vya kale kabisa kikiwa kimeanzishwa katika miaka ya 1,400.

Habari za kiutafiti zinaonesha kuwa tofauti ya kiimani kati ya makanisa ya kipentekoste na katoliki nchini humo, imechangia kwani baadhi wanaamini katika uponaji wa kimiujiza na wengine hawaamini  hivyo japo ni Wakristo.

Inadaiwa kuwa viongozi wa utawala katika Chuo hicho walifanikiwa kuufungua mtandao wake na kushtushwa na picha na matukio ya miujiza na alichukuliwa kama muasi wa imani, hivyo akachukuliwa hatua kali za kumtimua kazi.

Alipoulizwa na Shirika la CBN, kuhusu mkasa huo alisema: “Watu wanaruhusa ya kuamini imani nyingi yoyote, tena ya kishenzi, lakini wasifutwe kazi, mimi niliyefanya kazi kwa uaminifu kwa miaka 11, nafukuzwa kwa kumuamini Yesu na kazi zake.”

Chuo hicho ni miongoni mwa vyuo vikongwe zaidi nchini Ubelgiji  kikiwa kimethibitishwa na makao Makuu ya Kanisa hilo yaliyopo Vatican. Lakini kwa sababu Ulaya ya kisasa ina mfumo unaofanana unaosimamia vyuo vikuu, suala la imani limekuwa changamoto kubwa.

Alisema: "Kama ungeniuliza unataka upate mkataba mpya?,” Ningesema  `ndiyo`.  `Una tatizo lolote na wafanyakazi wenzako? Ningesema hapana, kila kitu kiko vizuri kwa hiyo hakukuwa na tatizo na juma moja baadaye nikatimuliwa, nikabaki  najiuliza, `nini kimetokea?."

kilichotokea ni chuo kikuu hicho kutofurahishwa na huduma ya kwenye mtandao ya Fernando yenye kuamini katika nguvu na uwezo utokanao na upendo. Hii ni pamoja na shuhuda za watu mbalimbali walioshuhudia kuponywa kwa uweza wa Mungu kupitia huduma hiyo.

Pauwels alisema,"Chuo kikuu kilikuwa kimeona baadhi ya vipande vya picha za video zinazoonesha watu wakiponywa na kisha kutoa shuhuda ambapo kwa mtazamo wa chuo watu hao waliitwa kuwa siyo wanasayansi.

Msemaji wa Chuo hicho katika mahojiano na CBN alisema: "Mtafiti wa mambo ya kisayansi  anaporuhusu dini kuchukua nafasi ya sayansi, anakiuka taratibu na kushusha hadhi ya chuo na vilevile anaondosha imani ya uongozi kwake kwamba ataweza kuwafundisha watu imani badala utafiti."

Hata hivyo, alisema: "Kama nimefukuzwa kazi kwa sababu ya kuamini kitu kisicho cha kisayansi kama hicho, kwamba Yesu Kristo bado anaponya, najisikia vizuri, lakini walichonifanyia siyo sahihi."

Msemaji wa chama cha kidemokrasia cha Kikristo, ambaye anafanya kazi katika Bunge la Flemish, Bw. Ward Kennes aliiambia CBN: "Nilishangazwa sana kwamba chuo kikuu cha kikatoliki, ambako nami ndiko nilikosoma, kinafanya mambo kama haya."

Rik Torfs, mfanyakazi katika kitivo kimojawapo chuoni hapo ambaye pia ni mwanahabari aliliambia  gazeti la Flemish la Standard: "Uhuru wa kidini una maanisha kuwa kila mtu yuko
huru kuamini kitu chochote apendacho au kinachomvutia."

Siku za hivi karibuni, Torfs aliteuliwa kuwa mkuu wa kitivo kimoja chuoni hapo na mapema kabla ya uteuzi wake   alipohojiwa na CBN alisema endapo atashika nafasi hiyo, angemrejesha Fernando Pauwels kwa kumkodisha kama mtaalamu mwalikwa.

Pauwels, ambaye ana moyo wa kujitoa kwa ajili ya Kanisa la Mungu, alisema anajisikia vizuri anapoteswa kwa ajili ya Kristo, lakini pia anataka wakristo wenye itikadi kama yake walindwe kutokana na ubaguzi kama huo.

"Siku moja nitasimama mbele za Bwana na atasema, umefanya vema, Hicho ndicho kinachotakiwa," alisema.

Bishop Zachary Kakobe na Don Moen katika semina Canada


Youth Talents Explosion Concert


Jeans & T-Shirt


Watoa Mil. 100 kulipia maisha baada kufariki

Kitendawili cha nini hatima ya maisha ya mwanadamu baada ya kufariki dunia, kinaendelea kuutesa ulimwengu wa wasomi tena waliotukuzwa kwa ubingwa wa kufikiri,safari hii kimewatatiza mabingwa wa falsafa  na utafiti wa maisha ya wanadamu katika Chuo Kikuu cha  Oxford, wakalazimika kulipa zaidi ya Milioni 100 ili miili yao itunzwe kitaalamu kwa kuwa wanaamini kuwa watarejea baadaye duniani.

Wasomi hao wakiongozwa na Profesa Nick Bostroma wamelazimika kutoa milioni 100, na kutia saini mkataba,na kampuni moja ili watakapokufa miili yao itunzwe kitaalamu hadi hapo roho zao zitakaporejea tena duniani.

Wataalamu hao katika utafiti wao wanadai kubaini bila shaka kuwa baada ya mwanadamu kufariki hukaa kwa muda na baadaye hurejea duniani na kuvaa miili kisha kuishi tena.Kwa sababu hiyo, walihofia kuwa kama watazikwa na miili yao kuoza basi watakaporejea wanaweza kujikuta katika miili ya ovyo na wakaishi maisha ya tofauti na walivyo sasa, jambo litakalowatesa na kuwanyima kufaidi uwezo walionao sasa.

Habari kutoka nchini humo zimeweka kuwa, tukio hilo la kwanza kufanywa na wabobevu wa elimu ya dunia, zimetokana na imani inayolenga kuwahakikishia wafu kurudi tena duniani, ingawa utafiti wao  unaokinzana na Biblia hauitaji kipindi cha marejeo ya miili.

Mbali na Profesa Nick Bostroma, ambaye pia ni Mkurugenzi wa taasisi inayojishughulisha na Maisha baada ya kifo, katika chuo hicho maarufu duniani, waliomuunga mkono ni wanataaluma wenzake ambao ni pamoja na  Anders Sandberg na Stuart Armstrong.

Prof. Bostman ametia sahihi mkataba wa kisheria  ili mwili wake uhifadhiwe kwa teknolojia maalum ambayo inahusisha kemikali zenye uwezo mkubwa wa kutunza miili isiharibike baada ya kufa,  huku Sandberg na Armstrong, wakisaini kuhifadhiwa kwa vichwa vyao pekee.

Wanaowadhihaki wanadai kuwa wamefanya hivyo kwa kuwa kwao vichwa vilivyonolewa vyema vyuoni, kuwa na maarifa mengi ndio vya thamani na sehemu zingine za miili wanaweza kuvaa vyovyote.Katika mikataba hiyo, wataalamu wameeleza kuwa, wakati wakisubiri kurejea tena duniani miili yao iwekwe kwenye kumbukumbu za kihistoria kwenye mji wa Michgani  ili vizazi  vijavyo viweze kubaini hali ya watu wa sasa.

Familia za wasomi hao wa falsafa zimeunga mkono mpango huo  wakiuelezea kuwa ni wenye heshima kubwa ndani ya jamii zao.Wataalamu wa kampuni iliyojitangaza kuwa na uwezo wa kuunda  mfumo wa kuhifadhi miili ya waliokufa, yenye makao yake katika Jimbo la Arizona, wanabainisha kuwa, wamekubaliana na hoja za wasomi hao na wamesema watavipulizia na kuvitunza vichwa hivyo kwa kemikali maalumu na kuwekwa katika eneo lenye baridi kwa manufaa ya vizazi vijavyo na tumaini la wahusika.

Profesa Bostrom kiongozi wa mpango huu ni miongoni mwa watu watukuka katika elimu ya falsafa akiwa tayari ametoa machapisho 200  yaliyozua mijadala  miongoni mwa wasomi na kumjengea heshima kubwa.
Miongoni mwa machapisho yake yaliyorejewa sana na wasomi katika mijadala ya kitaaluma ni Anthropic Bias (Routledge, 2002), Global Catastrophic Risks (ed. OUP, 2008), na Human Enhancement (ed.OUP, 2009). Kitabu chake kilichopo mbioni kuchapishwa kinachoitwa Super intelligence, kinasubiriwa kwa hamu huku vionjo vyake vikijikita kwenye imani ya wafu kurejea duniani.

Licha ya kujinyakulia tuzo ya (Eugene R. Gannon Award) inayotolewa kwa mtu mmoja anayechaguliwa kutoka duniani kote kutoka katika fani ya  Sanaa, Falsafa na hesabu katika  mwaka  2009, ametwajwa kuwa miongoni mwa mabingwa 100 wa kufikiri, wenye uwezo wa kutoa majibu ya yale yanayowatesa wengine.

Ni msomi ambaye amepata uwanja mpana wa kuzitambulisha kazi zake kupitia radio, magazeti na luninga, hivyo kuaminika sana na kujulikana katika ulimwengu wa waliosoma, hali inayowapa hofu wale wanaopinga imani yake ya kufa na kurejea baadaye kuvaa miili ya kibinadamu.

Kwa upande wake,Sandberg ni miongoni mwa watafiti kwenye taasisi hiyo ndani ya chuo cha Oxford, aliyejikita katika utafiti wa mustakabali wa sayansi na Teknolojia.

Bw.Anders ni mbobevu wa elimu ya Sayansi ya  Compyuta na uchunguzi wa ubongo wa mwanadamu na pia ni Injinia wa vifaa vya matibabu. Alipata shahada ya uzamivu  (Ph.D)  katika Chuo Kikuu cha Stockholm nchini Sweden,akijishughulisha haswa na mifumo ya kumbukumbu ya mwanadamu.

Dhana hiyo ya kuwa mwanadamu akifa atafufuka mwenyewe na kurejea tena duniani kuingia katika mwili inapingana na kweli ya Neno la Mungu  inayoeleza wazi kuwa baada ya mwanadamu kufa anasubiri kufufuliwa  na Bwana Yesu kwa ajili ya hukumu ya moto jehanamu kwa watenda dhambi na kuurithi  ufalme wa mbinguni kwa wale waliopokea wokovu.

Masanja Mkandamizaji aelezea fursa za vijana kuwekeza Mashambani.

Emmanuel Mgaya maarufu kama Masanja Mkandamizaji
Emmanuel Mgaya maarufu kama Masanja Mkandamizaji amesema kuwa vijana wanapaswa kufikiria namna ya kuwekeza mashambani kwenye fursa za kutosha kuliko kuendekeza majivuno yasiyo na msingi.

Akizungumza na Starehe Masanja alisema anafurahi kwani mwaka huu amefanikiwa kuvuna tani kadhaa za zao la mpunga katika shamba lake lililopo Mbarali Estate.

“Nimelimia Mbarali Estate namshkuru Mungu kwa kufanikiwa kuvuna mpunga wangu baada ya kuwekeza shamba lenye ukubwa wa ekari 15, huu ni uwekezaji mzuri unaotoa matunda kwa muda mfupi iwapo utahudumia shamba lako ipasavyo.”

“Vijana wengi wana nguvu na uwezo wa kuingia mashambani ila wanaendekeza ‘usharobaro’ kitu ambacho hakina mavuno kwao,” alisema Masanja aliyetumia mashine ya kisasa katika zoezi hilo.

Masanja ambaye pia ni mwimbaji wa kwaya ya New Jerusalem alisema: “Mimi ni mchungaji mtarajiwa lakini huduma yangu ya uchungaji nimeanzia kwenye kundi langu hili la Ze Komedy, kupitia hilo nina washirika wangu ambao natamani wawe kama mimi mchungaji wao wafuate nyayo zangu, naomba maombi ya watumishi wengine wamuombee Joti,” alisisitiza!

Kwa sasa, Masanja anahudhuria ibada katika kanisa la EAGT, Mito ya Baraka pia amefanikiwa kutoa nyimbo 10 za Injili na tayari album yake ya ‘Hakuna Jipya’ iko mitaani.

‘Mikutano ya Injili ruksa’ Askofu Dk. Bruno Mwakibolwa


Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste Tanzania PCT, Mkoa wa Dar es Salaam, limetegua kitendawili kilichokuwa vichwani mwa watanzania wengi siku zimepita, juu ya kuzuiwa kwa mikutano ya hadhara mara baada ya kutoa tamko lao juu ya suala hilo, hivi karibuni na kuzua sintofahamu, huku viongozi wa kisiasa nao wakizidisha utata.

Akisoma tamko hilo la Baraza la Maaskofu wa PCT, Mwenyekiti wa Baraza hilo, Askofu Dk. Bruno Mwakibolwa, alisema kuwa, Serikali haijazuia mikutano ya hadhara japo kuna vyombo vilivyoandika  hivyo.

“Mnamo tarehe 7-8 Mei Mwaka huu, kulifanyika mkutano wa viongozi wa dini za Kikristo na  Kiislam chini ya uongozi wa serikali ya Mkoa wa Dar es Salaam, ambao hata sisi tulishiriki,” alisema Askofu Mwakibolwa na kuongeza.

“Katika kikao hicho yalijadiliwa mambo mengi yaliyohusu amani, usalama na ustawi wa jamii. Aidha mwisho wa mkutano huo tulifikia maazimio 16, na kati ya maazimio hayo hakuna azimio lililositisha au kuzuia uenezaji wa dini kwa njia ya mikutano ya hadhara.

Bali kilichoafikiwa ni mihadhara ya kidini kufanyika kwa namna ambayo haisababishi uvunjifu wa amani, kuwabugudhi watu au kuingilia uhuru wa kuabudu wa watu wengine.

Kwa sababu hiyo, Baraza la Makanisa ya Kipentekoste Mkoa wa Dar es Salaam, limependa kuujulisha umma kwamba taarifa zilizoenezwa kwamba mikutano ya hadhara ya injili imepigwa marufuku si taarifa za ukweli, bali ni taarifa za uongo zilizopotosha ukweli wa yaliyo afikiwa.” alisema Dk. Mwakibolwa wakati akisoma tamko hilo.

Dk.Mwakibolwa aliweka wazi kuwa lazima injili ihubiriwe katika taifa la Tanzania ili watu wamgeukie Mungu na kuachana na utu wa kale,waishi maisha ya kumpendeza BWANA.

“Katika mikutano ya injili watu hatari wameokoka na kuachana na vitendo viovu, wezi wameacha wizi, mashoga wameacha kazi hiyo, majambazi wameacha ujambazi na sasa wanamtumikia Mungu hii ni kutokana na injili ya kweli isiyo na uchochezi wa aina yoyote inayohubiriwa na watu kuamua kugeuka,” alisema Mwenyekiti huyo wa PCT.

Hivyo akawataka watumishi wa Mungu,walioko maeneo mbalimbali ya taifa la Tanzania kuendelea kumtumikia Mungu kwa kuhubiri injili yenye lengo la kuwakomboa watanzania wanao potea dhambini.

Sambamba na hilo alisema, hata katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatoa uhuru wa watumishi wa Mungu kuhubiri injili, pasipo kubugudhiwa na mtu wa aina yoyote.

Hivi karibuni kumekuwa na taarifa ya watumishi wa Mungu kukamatwa hususani maeneo ya mikoani kutokana na kuhubiri mikutano ya injili ambapo Dk.Mwakibolwa alisema kuzuiwa kwa watumishi hao na kuzuiwa kufanya mikutano ni kwenda kinyume na sheria ya nchi.

Askofu David Mwasota ni Katibu wa PCT, akizungumzia suala hilo alisema kuwa, serikali haijazuia mikutano ya hadhara, bali mikutano yenye lengo la kuleta uchochezi ndiyo hairuhusiwi.

Katibu huyo akaongeza kuwa lazima watumishi wa Mungu wafanye kazi ya kuihubiri injili kupitia mikutano ili kuleta ukombozi katika taifa la Tanzania ili watu waachane uovu na kumgeukia Mungu aliye hai.

“Injili ndiyo uhai wa kanisa, sasa sisi tuzuie mikutano ya hadhara tutakuwa tumefanya nini, lazima injili ihubiriwe, injili ikizuiliwa hapo sasa hakuna haja ya kusajili makanisa, lazima tumtangaze Yesu aliye hai kupitia mikutano ya hadhara,” alisema Mwasota.

Mbali na hilo akawataka watumishi wa Mungu kujikita kuifanya kazi ya Mungu kwa bidii, ili kulikomboa taifa la Tanzania, ambalo hivi sasa linakabiliwa na changamoto lukuki, ikiwa ni pamoja na kuliombea.

The Annual Breakthrough Conference


Viongozi wa dini wamesifu rasimu ya katiba mpya.

 Askofu Msaidizi wa Jimbo Katoliki la Bukoba, Dk. Methodius Kilaini, alisema kupunguzwa kwa ukubwa wa baraza la mawaziri ni muhimu na kilio cha muda mrefu cha watu wengi na kuwa siyo Tanzania tu hata Kenya wamepunguza ukubwa wa baraza lao.

Kuhusu mgombea binafsi, alisema linafaa maana litawezesha vyama kuleta wagombea makini zaidi  na kuondoa tatizo la kuleta wagombea mashemeji au wajomba ambao wanakwamisha maendeleo ya nchi.

Alisema suala la rais atakayechaguliwa kulalamikiwa mahakamani ni muhimu, lakini hilo litapoteza umuhimu wake endapo kesi itakayopelekwa mahakamani itacheleweshwa.

Kuhusu suala la serikali tatu alisema binafsi angependelea serikali moja tu ila anajua ni vigumu sana kuwepo, lakini akasema kama siyo hivyo, muundo wa serikali tatu ni muhimu maana utawezesha Tanzania Bara kuzungumza masuala yao na Zanzibar pia, huku ya Muungano yakiachwa kuzungumziwa na serikali ya shirikisho.
 
Katibu Mkuu wa Umoja wa Makanisa ya Kipentekoste nchini (CPCT), Mch. David Mwasota

Kuhusu Spika wa bunge na naibu wake kutokuwa wabunge wala kutokana na vyama vya siasa, alisema linafaa maana litasaidia spika kuendesha bunge kwa mujibu wa sheria na taratibu zake bila upendeleo.

Aidha ,alipongeza kuwekwa kwa kipengele cha rais anayechaguliwa kupata kura zaidi ya kura asilimia 50 na kuwa hatua hiyo itawezesha kupatikana kwa kiongozi aliyechaguliwa na watu wengi.

Katibu Mkuu wa  Umoja wa Makanisa ya Kipentekoste nchini (CPCT), Mch.  David Mwasota, alisema rasimu ni nzuri na imezingatia matatizo na kero za wananchi na kwamba rasimu imeonyesha  kuondoa  mianya ya kuwagawa Watanzania.

“Matatizo yote yaliyokuwa yanawasumbua wananchi kwa muda mrefu  tangu Nyerere aondoke yamekuja vizuri ikiwa ni pamoja na masuala ya muungano, kwani kama kila nchi ina bendera na wimbo wake,” alisema na kuongeza:

“Sio kwamba mambo yote yamekamilika, hiyo ni generally tu (kwa mtazamo wa jumla). Na mambo mengine yaliyo ndani yake tunaona yamekaa vizuri. Mbali na kwamba ni jumla, lakini tunaiona nuru kwa mbali inaanza kutokea nchini.”

Hata hivyo, msemaji wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Mch. John Kamoyo, alisema kuwa ni mapema mno kutoa maoni kuhusu rasimu hiyo kwani ni siku moja tu imepita tangu kutangazwa kwa umma wa Watanzania.

Kamoyo alisema kuwa unahitajika muda maalum kwa viongozi kukaa na kupitia na kwa pamoja watatoa maoni kuhusu rasimu hiyo.

Occupy Conference 2013 "It is God's Time to Act"


Mauaji ya mtoto wa Mchungaji Mwimbaji

Utata mkubwa umegubika vifo vya mtoto wa Mchungaji mmoja wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God (TAG), na muumini mwingine wa kanisa hilo, vilivyotokea hivi karibuni na kuacha maswali mengi, yaliyoacha mguno mkali kwa familia na hata jamii kwa ujumla.

Kwa mujibu wa watu walioshuhudia tukio hilo, marehemu hao Utukufu Stefano na Yassin Pascal, walikutwa kwenye bwawa la  kubatizia  wakiwa uchi wa nyama, huku nguo zao na simu zikiwa pembeni.
Mchungaji Stefano Bugele, wa Kanisa la TAG, wilayani Sikonge, mkoani Tabora, akiongea na Jibu la Maisha, katika mahojiano maalumu; alisema kuwa siku ya tukio Mei tatu, mwaka huu, kijana wake huyo aliondoka nyumbani akichukua bomba la kupigia dawa akaenda kwenye bustani yao iliyopo umbali wa nusu Kilometa hivi.

Alisema kuwa baada ya kijana wake kwenda bustanini, yeye  aliongozana na Pascal kwenda kwenye msiba wa jirani na walipomaliza alimuuliza ikiwa ananafasi aungane na mwenzake kwenye kazi ya bustani.
“Unajua huyu Pascal ni muumini wangu wa kwanza nilipokuja kufanya umisheni hapa, na alipookoka alikaa nyumbani kwangu akawa kama mtu wa nyumbani, pia akapendana na mdogo wangu akamuoa hivyo akawa ni shemeji yangu. Na kwa kweli bado alisalia kuwa kijana wangu,” alisema na kuongeza:

“Nilipomwambia habari ya bustanini aliniambia kuwa hata yeye alipanga kunisaidia, nikachukua piki piki nikampeleka mpaka bustanini nikamkuta kijana wangu Utukufu anendelea na kazi, nikawaacha nikaondoka kwenda mjini kumpeleka kijana mmoja ambaye alipata ajali mbaya na kuumia mkono.”
Mchungaji huyo alisema kuwa, baada ya kumpeleka kijana huyo hospitali aliendelea na kazi zake kama kawaida na ilipofika saa  saba aliwapigia simu wakamwambia kuwa wanaendelea vyema na kazi.

“Mimi niliendelea na shughuli zangu na ilipofika saa mbili usiku nilipigiwa simu na kijana mmoja aliyekuwa na matatizo, nikaenda kumsaidia, ilipofika saa  tatu na dakika kadhaa mke wangu alinipigia simu akiniarifu kuwa mke wa Pascal alikuwa nyumbani akimsaka mumewe na wote walikuwa hawajarejea nyumbani hadi wakati huo,” alisema Mchungaji.

Alisema kuwa aliporejea nyumbani alijaribu kupiga simu lakini haikupatikana na alimuaga mkewe kuwa anaenda bustanini kuwatafuta, lakini mkewe akasema kuwa ni vyema waende wote, na kwa pamoja wakatembea hadi bustanini ambapo walistaajabu kukuta nguo zao na ndala na yebo yebo walizokuwa wamevaa, ingawa wenyewe hawakuwaona.

“Nilimwambia mke wangu twende kijijini kwa mke wa katibu wa kanisa tumuulize labda ana taarifa zao. Tulienda tukamgongea mama huyo na kumuelezea, akatuambia kuwa  majira ya  mchana alienda bustanini hapo kwa kuwa bustani yake nayo ilikuwa ikipuliziwa dawa na akawasifu  vijana hao kwa uchapaji kazi,”alisema Mchungaji na kuongeza:

“Mama huyo alituambia kuwa majira ya saa 11, jioni alipita tena hapo bustanini akitokea kwenye semina kanisani, akakuta nguo za vijana hao zikiwa zenyewe na hawakuwepo, kwa kuwa yeye ni msichana aliona kuwa pengine wamekwenda kuoga hivyo si vyema kuwasubiri kwani wanaweza kurejea wakiwa hawajavaa na akaondoka.”

Mchungaji Stefano, alisema kuwa baada ya maelezo hayo waliamua kurejea tena bustanini ambapo walichukua simu za vijana wao na kurejea kijijini ambapo walitoa taarifa kwa mwenyekiti wa kitongoji na hapo watu walianza kumiminika nyumbani kwake.
“Saa 12, alfajiri tuliondoka na kundi kubwa la watu kwenda bustanini kuwatafuta na tulipofika tu, tulistaajabu kuwaona wote wawili wakiwa ndani ya bwawa wakielea na huku wakiwa wameshafariki dunia. Nilipoona vile nilianguka na sikujua kilichotokea, hata walivyotolewa sikujua; nilipopata fahamu nilikuwa nyumbani na Polisi walishafika,” alisema  Mchungaji huyo  na kuongeza:

“Awali madaktari na Polisi waliwaangalia tu kwa mbali na kusema kuwa wamekufa maji tukazike, lakini alipofika Askofu wa TAG, Tabora akiwa na Afisa Upelelezi wa Mkoa waliambiwa warejee kwenye uchunguzi upya na wakafanya na kutoa taarifa ya kuruhusu mazishi yaendelee.”

Alisema ingawa inaelezwa kuwa walikufa maji lakini mimi nina mashaka kwa kuwa Utukufu alivuja  damu nyingi na hata walioosha maiti walisema wazi kuwa alikuwa na majeraha kichwani  ya kupondwa pondwa.
“Kwa kweli bado nafuatilia kwa makini tikio hili kwa kuwa kuna watu wamerusha habari mbaya za kunichafua. wametoa habari zao bila hata kuniuliza ,” alisema.

Mama mzazi wa Utukufu, Bi. Leah Amoni (Mama Mchungaji), akisimulia tukio hilo kwa uchungu alisema kuwa, wanamuachia Mungu aliye hakimu wa haki, lakini haamini kuwa kijana wake ambaye alikuwa akitegemewa kanisani kwa kazi ya Mungu alikufa kwa kuzama kwenye maji machache yasiyoweza kumzamisha hata mtoto wa miaka 10.

Mama huyo, anasema kuwa tukio hilo ni pigo kwao na kanisa, kwani licha ya mwanaye Utukufu kuwa mpiga vyombo na mwimbisha sifa, mwenzake waliyeuawa pamoja (Pascal) alikuwa Mwenyekiti wa Kwaya ya Kanisa.

“Wakati mmoja alikuwa akitoka damu nyingi mwingine alikuwa amekabwa shingo ikavimba, hali ambayo inaashiria kuwepo kwa mkono wa mtu. Hata hivyo tunamuachia Mungu yeye ndiye hakimu wa haki,” alisema.
Makamu Askofu wa Kanisa la TAG, Jimbo la Tabora, Sadoki Bukuri, alisema kuwa wamelipokea tukio hilo kwa masikitiko makubwa, lakini kwa kuwa Polisi walishafanya kazi yao na kutoa kibali cha kuwazika marehemu wameliacha na kuendelea na shughuli zao kama kawaida.

“Mimi nami nilikuwa eneo la tukio, yaani kwenye bwawa wakati wa kuwatoa nilishiriki pia, lakini kweli niliona utata kwa kuwa, walikuwa wakitoka damu jambo ambalo ni ajabu kwa mtu aliyekufa kwa kunywa maji (kuzama),” alisema na kuongeza:
“Kanisa linaendelea na taratibu zake kama kawaida, ila mchungaji amepeleka maelezo yake kituoni na nadhani watafuatilia kujua ukweli wa jambo lenyewe.”

Utata zaidi wa tukio hilo unasababishwa na mfululizo wa matukio ya kuuawa kwa watumishi wa Mungu na kushambuliwa kwa makanisa Tanzania wakati huu.
Baadhi ya wakazi wa Tabora wanaeleza kutolewa hasa ukweli kuhusu hali hii na wanahitaji uchunguzi wa kweli ufanyike kama yanavyofanyika matukio mengine.