Hatimaye Majaji wa rufaa ya kifo cha Yesu watajwa.

Hatimaye Mahakama ya Kimataifa ya Haki “International Court of Justice (ICJ)” yenye makazi yake mjini ‘The Hague, Uholanzi imeteua jopo la majaji watakaosikiliza rufaa ya kihistoria na yenye utata mwingi, ya kesi na hukumu ya Bwana Yesu Kristo, miaka zaidi ya 2000 iliyopita.

Mwanasheria mwenye makeke mengi ni, Bw. Dola Indidis, amefanikiwa kukidhi matakwa ya mahakama hiyo hivyo kuipokea rasmi kesi yake na hivyo kuundwa kwa jopo la majaji wa kusikiliza kesi hiyo, hatua ambayo inaelezwa kuwa ni mafanikio makubwa.Taarifa fupi ya mahakama hiyo iliyotolewa wiki kadhaa zilizopita ilisema kuwa, kesi hiyo itapangiwa rasmi tarehe ya kusikilizwa kulingana na utaratibu wa mahakama hiyo.
Mwanasheria wa nchini Kenya , Bw. Dola Indidis

Awali kesi hiyo ilisikilizwa na mahakama ya Kenya kwa miaka mitatu kabla ya kuomba aipelekeke ICJ, kwa kuwa ndiyo yenye mamlaka ya kusikiliza kesi zinazohusu taifa moja dhidi ya lingine au watu wa mataifa tofauti. Katika mahakama kuu ya Kenya, mjini Nairobi, mwanasheria huyo anayedai kuwawakilisha marafiki wa Yesu alitumia vifungu namba  No. 965  vya katiba ya zamani ya Kenya.

Akielezea furaha yake baada ya kesi yake kupokelewa, Bw. Dola alisema kuwa, moyo wake unafuraha baada ya kuwasiliana na mahakama, na kuambiwa kuwa jopo la majaji limeundwa na atajulishwa kuhusu tarehe ya shauri lake kusikilizwa na hati ya kuitwa kortini kwa mataifa ya Itali na Israeli.

Alisema kuwa,  japo anakumbana na madai mengi kutoka kwa wale wanaosema kuwa Yesu alijitoa mwenyewe kuufia ulimwengu, hivyo kupata mateso ili kubeba dhambi za ulimwengu, lakini ukweli unasalia kuwa Yesu alikuwa mwanadamu; alizaliwa Bethlehemu,  mbele za mashahidi akaishi na kufanya kazi  kama wanadamu wengine kabla ya kuzushiwa unafiki na kuuawa kinyama.

“Najua wengi hawanielewi kwa kuwa wanamchukulia Yesu katika sehemu moja tu ya uungu, hawaangalii alizaliwa akaishi akila na kunywa, hivyo alistahili kutendewa kibinadamu,”alisema wakili huyo na kuongeza:“Tatizo la watu wengi ni kushindwa kutofautisha  baina ya mambo ya kiroho na haki ya kimwili, wengi hawajui kuwa Yesu alijihusisha na masuala ya kijamii, alilipa hata kodi ya serikali ya Rumi, walipopokea kodi yake si walijua ni raia wa Rumi anayestahili kulindwa na sheria, lakini alitendewa unyama wa kutisha.”Alifafanua kuwa anataka dunia ifahamu kuwa, Yesu hakuwa na hatia na hivyo hakuwa na kosa wala dhambi kama Biblia inavyosema, naamini kesi yangu itawafanya wanaomtuhumu na hata kumdharau kujua ukweli kuwa hakuna anayeweza kumpata na hatia ya haki.

 
Kisha anaongeza: “Kabla ya kwenda mahakamani nilifanya ziara ya Israeli kukusanya ushahidi kutoka katika nyaraka rasmi za kale zenye ushahidi wote unaoweza kuwatia hatiani warumi na wayahudi waliopo leo, kwa kadiri mambo yanavyokwenda furaha yangu inaongezeka na najua siku moja wanaoniona mwenda wazimu watatoka barabarani kushangilia ushindi tukiinua bendera ya Yesu hadi juu.”

Kwa mujibu wa Gazeti la Daily Monitor la Uganda, Mwanasheria huyo alishasafiri hadi Italia akachunguza na kupata ushahidi mwingi wa kudhihirisha kuwa sheria za Rumi zenyewe zilikiukwa na Jaji Pontio Pilato (Pontius Pilate), kwani alipotamka kuwa haoni hatia yeyote  kwa Yesu ilimlazimu amuachie huru na si kumtoa kwa wayahudi wamuue tena kwa adhabu ya kirumi.

Washtakiwa kwenye kesi hiyo ni  utawala wa Rumi (Emperor of Rome 42 BC-37AD), Pontius Pilate (Governor of Judea), kuhani mkuu wa Uyahudi Annas, viongozi wa dini ya kiyahudi na waalimu wa sheria, Mfalme  Herode,  taifa la Israeli na Jamhuri ya Italia.
Katika ufafanuzi wa hati ya mashtaka, kuhani mkuu anatuhumiwa kumkamata Yesu, akampiga kisha akampeleka katika mahakama ambayo ni dhaifu na isiyotenda haki akihofia kuwa Yesu atatatiza utawala wake hasa wakati wa pasaka ambao wayahudi walikusanyika Yerusalemu.

Mhadhiri  katika vyuo vikuu nchini na mjenzi makini wa hoja, Prof. Malise Kaisi, akiongea na chanzo cha habari hii katika mahojiano maalumu  kuhusu kesi hiyo alisema kuwa,  kwa mtazamo wa haraka mlalamikaji anaonekana kama mwenda wazimu kwa kuwa  yapo maandiko mengi ya Biblia yanayoonesha kuwa Yesu alijitolea mwenyewe kufa msalabani.

Kifo chake kilitabiriwa miaka 700 kabla ya kutokea na alipokuwa anaelekea kwenye pasaka aliwaambia wanafunzi wake kuwa anakwenda Yerusalemu, atakamatwa na kusulubiwa  atakufa na kufufuka siku ya tatu.

“Maandiko yanatuonesha kuwa, wakati ambao Yesu hakutaka akamatwe walipojaribu kumsukuma alipita kati kati yao  na wala hawakumuoana, na wakati wake wa kutimiza kusudi la kuja kwake ulimwenguni lilipofika aliruhusu afe. Tukumbuke kuwa Yesu alisema ataitwaa Roho yake na kuitwaa tena,”alisema Profesa Kaisi.

Prof. Kaisi anasema kuwa,  kwa sasa ulimwengu umenufaika zaidi na kifo cha Yesu kuliko madhara, hivyo itakuwa ni shida kuishawishi mahakama  kuona umuhimu wa mashtaka  hayo.Mmoja wa mawakili wa mahakama kuu, Kenedy Mushi, alisema kuwa,  miongoni mwa mambo yatakayoleta utata kwenye kesi hiyo ni udhibitisho kuwa Yesu amekufa au yu hai, kwani kaburini alipozikwa  hakuna mabaki wala mifupa.

Lakini akasema kuwa, huenda mlalamikaji akatumia ushahidi wa taarifa rasmi iliyotolewa na serikali kuwa  mwili wa Yesu uliibwa na wanafunzi wake.

No comments:

Post a Comment