Wachungaji 14 waondolewa Moravian

Kanisa la Moravian Jimbo la Kusini, limetangaza kuwafukuza kazi wachungaji wake 14 na makatibu wanne wa idara mbalimbali kwa kosa la kuchochea vurugu ndani ya kanisa hilo.

Uamuzi huo ulifikiwa jana na Halmashauri Kuu ya Jimbo la Misheni Mashariki na Zanzibar baada ya wachungaji hao kujitangazia halmashauri yao mpya, wakijitenga na uongozi ndani ya kanisa.

Pamoja na kuwaondoa wachungaji hao, uongozi huo wa jimbo, umefanya mabadiliko ya uongozi katika Wilaya ya Morogoro na kuwateua wachungaji wengine kadhaa kuziba nafasi zilizoachwa wazi na wachungaji waliofukuzwa.

Uamuzi huo umekuja wakati aliyekuwa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Jimbo la Mashariki na Pwani ya Kanisa la Moravian Tanzania, Clement Fumbo na wenzake saba wakiwa wamefungua kesi namba 222 Mahakama Kuu ya Tanzania, dhidi ya Bodi ya Wadhamini wa Kanisa la Moravian Jimbo la Rungwe kupinga kuvuliwa madaraka na kusimamishwa kazi.

Katika kesi hiyo iliyopangwa kuendelea kusikilizwa Februari 6, mwaka huu mbele ya Jaji Augustini Mwarija, Fumbo na wenzake saba wanapinga kuondolewa madarakani na kusimamishwa kazi na wanaiomba mahakama iamuru walipwe Sh500 milioni kama fidia na gharama ya kesi.

Kadhalika uamuzi wa kufukuzwa kwa wachungaji hao umefanywa wakati Mchungaji Fumbo akidai kwamba yeye bado ni mwenyekiti halali na kutangaza halmashauri yake mpya, jambo ambalo uongozi wa Kanisa la Moravian unasema ni kinyume cha katiba wa kanisa hilo.

Akitoa taarifa ya hatua hiyo mbele ya waumini wa kanisa hilo lililoko Ushirika wa Mabibo jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa Jimbo la Misheni Mashariki na Zanzibar, Adolf Mwakanyamale, aliwataja wachungaji waliofukuzwa kuwa ni pamoja na mwenyekiti wa Wilaya ya Kaskazini, Alinanuswe Mwakilema.

Wengine na nyadhifa zao kwenye mabano ni Noel Mwakalinga,(Mjumbe wa Halmshauri Kuu), Fanny Ndemange (Katibu wa Idara ya Kina Mama), Angelina Mwamakula (Mchungaji Msaidizi Ushirika wa Kimara) na Mariamu Kasendeka wa Ushirika wa Pugu Kajiungeni.

Wachungaji wengine na sharika zao kwenye mabano ni Tumaini Mwakijale (Tanita) Mosted Kibona (Kitunda), Eliza Kipesile (Kawe), Lugano Anganisye (Mwenge), Baraka Mwakijale (Mlandizi), Azaria Lwaga (Segerea) na Fredy Mwakyusa wa Usharika wa Kiwalani.

Katibu huyo aliwataja wakuu wa idara wanne waliofukuzwa kuwa ni Mchungaji Anyasime Kasebele (Uwakili), Emmanuel Mwaijande (Kwaya), Hezron Mwangaja (Uinjilisti) na Silas Mwakibinga (Miradi na Maendeleo).

“Tumeamua kuwaita pia wachungaji wetu wastaafu, lengo likiwa ni kuziba mapengo yote yaliyotokana na ndugu zetu ambao wameamua kuasi na kujitangazia kanisa lao,” alisema Mchungaji Mwakanyamale.

Source: Mwananchi

No comments:

Post a Comment