Mchugaji Mtikila ashinda kesi iliyokuwa inamkabili.

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, jana imemuachia huru Mchungaji na Mwenyekiti wa Chama cha Democratic Party (DP), Mchungaji Christopher Mtikila aliyekuwa anakabiliwa na mashtaka ya kutoa nyaraka za lugha ya uchochezi kuhusu Rais Jakaya Kikwete na kumiliki hati hizo isivyo halali baada ya upande wa Jamhuri kushindwa kuthibitisha mashtaka dhidi yake.

Hukumu hiyo ilisomwa jana na Hakimu Mkazi, Mfawidhi, Illivin Mgeta baada ya ushahidi uliotolewa na upande wa Jamhuri bila kuacha shaka mahakama imemuona hana hatia.

“Bila kuacha shaka mahakama hii imepitia ushahidi uliotolewa na upande wa Jamhuri haujamgusa mshtakiwa…mashahidi wanne walitoa ushahidi upande wa mashtaka pamoja na  kuwasilisha kielelezo cha maelezo aliyotoa Mtikila Polisi wakati akihojiwa,”
 
Mchungaji na Mwenyekiti wa Chama cha Democratic Party (DP) Christopher Mtikila
Aliongeza kuwa “Katika kielelezo hicho hakuna mahali ambako mshtakiwa alipendekeza Rais Jakaya Kikwete ang’olewe madarakani bali Mtikila alisema kwamba wananchi wasiipigie kura CCM katika uchaguzi lakini hakuwashawishi kumng’oa Rais Kikwete madarakani.”

Alisema katika ushahidi uliotolewa na Jamhuri unadai kwamba mshtakiwa alisema Rais Kikwete anaingiza Uislamu katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwamba anauangamiza kabisa Ukristo hivyo Wakristo waungane kumweka Mkristo Ikulu.

Alisema ili mshtakiwa atiwe hatiani kwa uchochezi lazima kuwepo na athari zilizojitokeza kutokana na nyaraka hizo zilizodaiwa kwamba za uchochezi lakini hakuna ushahidi kama huo uliotolewa mahakamani hapo na Jamhuri.
 


“Kwa maoni yangu hakuna ushahidi wa kumtia hatiani mshtakiwa kwa mashtaka aliyoshtakiwa nayo hivyo mahakama inamwachia huru…hakuna ushahidi kwamba maneno ya Mtikila yaliamsha hisia za Wakristo na Waislamu,” alisema Hakimu Mgeta.

Baada ya mahakama kumwachia huru Mtikila akiwa bado kizimbani alisikika akisema ‘haleluyaa’ na baadhi ya watu wanaodhaniwa kuwa waumini wake waliitikia ‘amen’.

Alisema hukumu iliyotolewa aliitegemea na kwamba hakuwa na mashaka na hakimu aliyesikiliza kesi hiyo.

Mara baada ya kutoka ukumbi namba mbili wa mahakama hiyo, Mchungaji Mtikila alijikuta katika wakati mgumu baada ya Polisi waliotanda mahakamani kutaka kumkamata na kumpeleka Polisi kwa ajili ya mahojiano kwa tuhuma za kumtishia kumuua kwa maneno, Gotam Ndunguru maeneo ya Kimara jijini.

Askari alipomwambia anatakiwa kukamatwa Mtikila alisema alikwishazungumza na Mkuu wa Kituo cha Polisi Mbezi na kumfahamisha kwamba alikuwa mahakamani hivyo atakwenda leo.

Katika kesi ya msingi, Mtikila alikuwa anadaiwa kuwa kati ya Januari mwaka 2009 na Aprili 17, mwaka 2010 jijini Dar es Salaam, kwa nia ya uchochezi alitawanya kwa umma nyaraka zilizosema 'Kikwete kuuangamiza ukristo', 'wakristo waungane kuweka mtu Ikulu.’

No comments:

Post a Comment