Kanisa la Waadiventist lalaani dhidi ya tukio la kuharibiwa kwa Nyumba za ibada.

Kanisa la Waadventista Wasabato limetoa tamko rasmi dhidi ya tukio la kuharibiwa kwa jengo la ibada la kanisa hilo lililoko Mbagala, jijini Dar es Salaam na kuchomwa moto kwa makanisa mengine ya Kikristo na watu wanaodaiwa kuwa ni waumini wa Kiislamu.

Akitoa tamko hilo mbele ya waandishi wa habari mjini Morogoro jana, Askofu Mkuu wa Kanisa hilo Jimbo la Mashariki mwa Tanzania, Mark Malekana, alitaka serikali kulichukulia suala hilo kwa uzito wa kipekee.

Alisema licha ya kanisa hilo licha ya kupongeza kauli za viongozi wa madhehebu mengine ya dini na serikali za kukemea na kulaani viendo hivyo, lakini viongozi wa dini ya Kiislam nao wanapaswa kuwachukulia hatua za kinidhamu waumini wao wanaohatarisha amani .


“ Lazima hawa viongozi wa dini ya Kiislam wawachukulie hatua hao waumini ambao wameanza kuharibu amani ama sivyo jamii itakuwa na picha isiyo sahihi,” alisema.

Askofu huyo alisema matukio ya kushambulia na kuharibu majengo matakatifu ya ibada ya Kikristo yamekuwa yakijirudia mara kwa mara na hata kusababisha wasiwasi kwa waumini wa dini hiyo, jambo ambalo likiachwa liendelee linaweza kuharibu amani nchini.

“Kanisa halikufurahishwa kabisa na kitendo cha mtoto kudhalilisha kitabu kitukufu cha Kuran na nailipongeza Jeshi la Polisi kwa hatua zilizochukuliwa za kumuweka kituoni mtoto huyo kwa uchunguzi zaidi na kwa usalama,” alisema.

Aliongeza: “Kitendo cha kukamatwa na polisi kinaonyesha jinsi dola isivyochukulia kirahisi mambo yayoweza kuvuruga amani miongoni mwa jamii. Kwa kweli kitendo cha mtoto huyo ni cha aibu.”

Alisema kuwa bado kanisa lake linalaani vitendo vya watu wazima wenye kujua sheria za nchi, tena watu wa kiroho kuamua kuchukua hatua mkononi kwa kuvamia kituo cha polisi na kufanya uharibifu wa makanisa ambayo hata hayakuhusika na kitendo kilichofanywa na mtoto huyo.

“Kwa kweli vitendo hivyo havikupaswa kabisa kutendwa na watu wanaomcha Mungu, kwani mcha Mungu ni mtu anayetegemewa kuwa muhimili wa amani katika jamii na kutokana na hali hiyo, ninawaomba pia viongozi wa dini ya Kiislam wawachukulie hatua za kinidhamu hawa waumini wao wanaohatarisha amani yetu ama sivyo jamii itakuwa na picha mbaya isiyo sahihi,” alifafanua Askofu Malekana.

Askofu huyo alisema kuwa kanisa lake limefarijika kwa kauli zilizotolewa na viongozi mbalimbali akiwAmo Rais Kikwete; Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Mecky Sadiki; Kamanda wa Polisi Kanda na Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova na Sheikh Mkuu wa Dar es Salaam kwamba zinazooneshwa kukerwa na matendo hayo na kuwataka waamini wa dhehebu hilo na Watanzania kwa ujumla kuwa wavumilivu wakati serikali ikishughulikia suala hilo.

Alisema Kanisa la Waadiventista Wasabato haliwezi kutafuta haki kwa kuvunja sheria, bali linapoona kuwa halitendewi inavyostahili, huitafuta haki kwa mujibu wa sheria.

Katika vurugu zilizotokea Oktoba 12, Mbagala jijini Dar es Salaam, jumla ya makanisa saba yalichomwa moto na mengine kuharibiwa na kikundi cha watu wanaotumia kivuli cha dini ya Kiislam kufanya vurugu hizo.

No comments:

Post a Comment